HOTUBA YA RAISI IMEVURUGA MWELEKEO HABARI KAMILI HII HAPA by nasanyo fortnine

Kaimu Mwenyekiti wa Jukata, Hebron Mwakagenda
 
Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), limesema hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa wiki iliyopita kuzindua  Bunge Maalum la Katiba, imevuruga mwelekeo wa mjadala  wa rasimu bungeni humo.
 
Aidha, jukwaa limebaini kuwa hotuba hiyo imeleta mgawanyiko kiitikadi na kimisimamo miongoni mwa wajumbe  bungeni, hususan katika suala la muundo wa serikali na Muungano kwani kuna wanaounga mkono muundo wa serikali mbili na wengine wakitaka  tatu.
 
Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Kaimu Mwenyekiti wa Jukata, Hebron Mwakagenda wakati akizungumza na wanahabari, kuhusu mwenendo wa bunge hilo.
 
Alisema  Tume ya Mabadiliko ya Katiba, iliyokuwa chini ya Mwenyekiti Jaji Joseph Warioba iliundwa na Rais Kikwete, hivyo hakupaswa kuonyesha msimamo wake kuipinga rasimu hiyo katika baadhi ya maeneo.
 
“Kitendo cha Rais kutumia sehemu kubwa ya hotuba yake kuzungumzia muundo wa serikali mbili hakikuwa  sahihi. Ifahamike kuwa kiutafiti haiwezekani kuwahoji watu wote. Matokeo ya takwimu yaliyotolewa na Tume ya Jaji Warioba yalikuwa ni ya kisayansi kwani walikusanya maoni kwa kutumia sampuli, na watu zaidi ya laki tatu walihojiwa,” alisema Mwakagenda.
 
Akizungumzia ubishani uliopo baina ya wajumbe juu ya kutumika kwa kura ya wazi au siri, Mwakagenda alisema kinachopaswa ni kufikia maridhiano ya kura ipi itumike.
 
Aidha aliongeza kuwa mwelekeo uliopo sasa bungeni, unaonyesha kutopatikana kwa katiba mpya, bali ni upotevu wa muda na rasilimali kwani zimeshatumika Sh bilioni 80 za walipa kodi, tangu mchakato ulipoanza.
 
Aliongeza kuwa  iwapo bunge hilo litaendelea kujadili mambo yasiyo na tija, kuzomeana, kubezana na kubishana, Jukata litawaongoza wananchi kulifunga bunge hilo, kwa kutumia ibara ya 8 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

0 comments:

Copyright © 2014 NASANYO BLOG