DARAJA LA DUMILA LILILO BOMOLEWA NA MAFURIKO LAKAMILIKA habari kamili iko hapa isome by tuntu baby

WAZIRI wa Ujenzi Dk.John Magufuli (wa pili kulia), akiruhusu magari kupita katika daraja la Mto Mkundi jana baada ya matengenezo ya tuta la daraja hilo kusombwa kwa maji kutokana na mafuriko katika tarafa ya Magole wilayani Kilosa Mkoani Morogoro. Kulia ni Mkuu wa kikosi cha Usalama Barabarani mkoani Morogoro, Boniface Mbao,
 
 
 
Mawasiliano  ya barabara kati ya Morogoro, mikoa ya kanda  ya ziwa na nchi jirani  yamerejea, baada ya  Wizara ya Ujenzi kukamilisha ujenzi wa tuta la daraja la Mto Mkundi  lililozolewa na mafuriko mapema wiki hii.

Ili kukamilisha kazi hiyo, Waziri wa  Ujenzi Dk. John Magufuli,  alilazimika kukesha na wataalam wa wizara hiyo kusimamia ukamilishaji  ujenzi wa tuta la daraja la muda la mto huo lililoko wilayani Kilosa mkoani Morogoro.

Ujenzi huo ulikamilika jana saa 4.45 asubuhi  na magari zaidi ya 5,000 yaliyokuwa yamekwama  kuanza kuruhusiwa kupita.

Baada ya kubomoka eneo la barabara hiyo, mabasi na magari madogo yenye uzito wa pungufu ya tani saba, yalitumia barabara ya Melela kuelekea Kilosa hadi Dumila na hadi sasa yanaendelea na njia hiyo.

Malori makubwa yaliyokwama yalianza safari jana kwa kuruhusu lori moja kupita. 

Alhamisi wiki hii, Waziri  Magufuli alipofika kwa mara ya kwanza katika eneo hilo, alihidi kukesha  mpaka ujenzi wa tuta hilo utakapokamilika.

Dk. Magufuli alisimamia ujenzi wa daraja hilo na  kuhakikisha kuwa linakamilika ndani ya saa 24 hivyo kurejesha mawasiliano ya  barabara kati ya  Morogoro na mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani.

Pamoja na Waziri  Magufuli, wengine waliokuwamo katika usimamizi huo ni  Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Joseph Nyamuhanja, Kaimu Mkurugenzi wa Barabara Ven Ndyamukama, Meneja wa Wakala wa Taifa wa Barabara (Tanroads)  Morogoro, Doroth Mtenga pamoja na wahandisi wa ujenzi wa mikoa ya Dodoma, Pwani na Dar es Salaam.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda baada ya kutembelea eneo la mafuriko Jumatano wiki hii ili kujionea athari za mafuriko hayo, aliahidi serikali itarudisha mawasiliano ya barabara hiyo kesho.

Akizungumza mara baada ya kukamilika kwa ujenzi huo na kuruhusu magari ya mizigo yaliyokwama kwa  siku tatu baada ya mafuriko hayo kuzoa tuta la daraja,Waziri Magufuli alisema alilazimika kukesha kusimamia ujenzi huo ili kuokoa uchumi wa nchi kwani daraja hilo ni  kiungo kikubwa kinachounganisha mikoa  na nchi jirani.

“ Nyote ni mashahidi hapa haya maji yalikuwa ni balaa, niliwaambia kuwa kesho magari yataanza kupita lakini kuna watu walinibishia na wengine wakaniambia naleta porojo niondoke zangu, lakini si leo tunafungua hii barabara na magari yanapita kama kawaida,” alisema Waziri Magufuli na kushangiliwa na madereva waliokuwa wanalala kulinda shehena na magari yao.

Alieleza kuwa mafuriko hayo yalisababisha kuharibika kwa tuta la daraja lenye  mita 50 kwa upande wa Morogoro na mita 20 kwa upande wa Dodoma hali ambayo endapo jitihada zisingechukuliwa barabara hiyo ingeathiri uchumi,

Usafirishaji wa shehena na  mafuta kwenda Congo, Zambia, Rwanda na Burundi.

Kazi hiyo ilikuwa imalizike Jumapili kutokana na ugumu wake, lakini wameikamilisha ndani ya saa 24 na hivyo kuanza kupita kwa magari hayo.

Alisema magari yanayopewa  kipaumbele ni yale yanayotoka upande wa Morogoro kuelekea Dodoma kwa kuwa ndiyo yenye mizigo ya mafuta na bidhaa nyingine kuelekea mikoa mingine na nje ya nchi.

Aliwataka madereva  kuacha kuzidisha uzito uliwekwa wa tani 56 ili kuokoa madaraja na barabara.

Kwa upande wao, madereva wa malori yaliyokwama  barabarani  walimteua Mwanyekiti Enest Shekif kuwawakilisha katika ufunguzi huo.

Akizungumza alimpongeza Waziri Magufuli kwa jitihada hizo alizofanya na kueleza kuwa ameonyesha kuwa si wa kubahatisha.

“ Nimetumwa na madereva wenzangu zaidi ya 5,000 tuliokwama hapa kwa siku mbili, mwanzoni tulijua hii ni kazi ya wiki ndiyo tutapita na alikuja Waziri Mkuu alisema mpaka Jumapili njia itafunguliwa ,lakini ulipokuja wewe tukawa na imani ni kweli leo tunapita ndani ya masaa 24.”

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo alimuomba Waziri Magufuli kwenda kuzungumza na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe kuipitia mikataba ya madereva wa malori kwani wanawanyonya na kulipwa Sh 150,000 kwa safari wakati mikataba wanayoiwasilisha serikali  inaonyesha kuwa wanalipwa 600,000  by tuntu baby


TOA MAONI YAKO HAPA CHINI...

0 comments:

Copyright © 2014 NASANYO BLOG