Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uratibu na Uhusiano), Stephen Wassira
akizungumza kwenye mdahalo uliofanyika jijini Dar es Salaam jana. Kulia
ni Mbunge wa Singida Mashariki(Chadema) Tundu Lissu na katikati ni
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Stephen
Wassira akiwakilisha CCM, Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, jana walitoana jasho katika
mdahalo wa Katiba ulioandaliwa na East African Business and Media
Institute.
Mdahalo huo uliohudhuriwa na watazamaji wapatao
500, ulikuwa na mada inayosema: ‘Nani anakwamisha Upatikanaji wa Katiba
Mpya.’ Kila upande ulitumia fursa hiyo kutupa shutuma kwa mwingine huku
jazba na kelele vikitawala miongoni mwa waliohudhuria.
Hata hivyo, suala la muundano wa serikali ndiyo
uliochukua nafasi kubwa katika mdahalo huo huku Umoja wa Katiba ya
Wananchi (Ukawa) ukiishutumu Serikali ya CCM kuwa ndiyo kikwazo cha
upatikanaji wa Katiba Mpya nayo ikitupa mpira huo kwa Ukawa kwa kitendo
chake cha kutoka katika Bunge Maalumu la Katiba.
Profesa Lipumba alisema wahafidhina wa CCM ndiyo
waliomshauri Rais Jakaya Kikwete abadilike kimsimamo kuhusu upatikanaji
wa Katiba Mpya.
“Rais Kikwete alikuwa na nia njema kabisa kuhusu
Katiba Mpya lakini wahafidhina wa CCM wanaopenda madaraka walipoona
muundo wa serikali tatu wakambana naye akabadilisha msimamo, tunamwomba
abadilike, nchi hii ni yetu sote ili tupate katiba ya wananchi,”
alisema.
Lissu aliongeza kwa kusema kuwa anayekwamisha
upatikanaji wa Katiba Mpya ni CCM ambao wanaweka maoni yao badala ya
kujadili rasimu iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ambayo ndiyo
maoni ya wananchi.
“Hatuwezi kurudi kwenye Bunge Maalumu la Katiba
kwenda kujadili rasimu ya CCM kwa sababu wanaonyesha hawana nia ya
Katiba Mpya, bali wanataka kuwadanganya Watanzania, watawadanganya
wananchi kwa kuleta Katiba ileile ila ikiwa na rangi tofauti,” alisema
huku akishangiliwa.
Alisema Ukawa hawawezi kushiriki katika
udanganyifu wa aina hiyo na kwamba wameamua kuwaachia CCM ili wananchi
waweze kuwahukumu kwa uovu watakaoufanya.
Alisema kati ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba
katika Kundi la 201, wajumbe 166 ni wana CCM walioteuliwa ili kuongeza
idadi ya watu.
“Humo kuna viongozi wa dini mashehe na maaskofu na
waganga wa kienyeji ambao ni wana CCM ili wapitishe Katiba yenye
masilahi yao binafsi,” alisema.
Hata hivyo, Wassira alisema hoja za Ukawa hazina
mashiko na kumtaka Lissu kuwaomba radhi masheikh na maaskofu kwa kuwa
hawakuteuliwa na Rais kutokana na kuwa wanachama wa CCM, bali ni
mapendekezo ya taasisi wanazozitumikia.
“Namwomba Tundu Lissu akawaombe radhi masheikh na
maaskofu kwa sababu kundi hili liliteuliwa kutokana na mapendekezo ya
wahusika wenyewe pasipo shinikizo la Rais. Hapakuwa na uwezekano wa Rais
kuwatambua wana CCM ili awateue wanaofaa. Kama ana ugomvi na Kingunge
Ngombale Mwilu aseme.”